Raia wa Rwanda ateswa na kuachiliwa Uganda


 Raia wa Rwanda ateswa na kuachiliwa Uganda

Mkimbizi mmoja raia wa Rwanda ambaye alitoweka nchini Uganda wiki iliyopita amepatikana akiwa hana ufahamu baada ya kuteswa.

Maafisa wa serikali ya Uganda wanasema kuwa waliomteka Pascal Manirakiza, walimdhulumu kabla ya kumuacha karibu na eneo la makaburini mjini Kampala.
Bwna Manirakiza, alikuwa mmoja wa raia wa Rwanda ambao waliiambia BBC kuwa wanatafuta hifadhi nchini Uganda mwezi uliopita.

Wakimbizi hao wameishutumu jeshi la serikali ya Rwanda kwa kuwasajili kwa lazima kupigana katika vita vinavyoendelea Mashariki mwa Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
Hata hivyo jeshi la Rwanda limepuuzilia mbali madai hayo, na kusema watu hao wakitoa madai hayo ili kupewa hifadhi nchini Uganda.

Wiki iliyopita Umoja wa Mataifa uliitisha kufanyika kwa uchunguzi kufuatia kutekwa nyara kwa wakimbizi watatu raia Rwanda nchini Uganda.

Rwanda inakana kuhusika

Serikali ya Rwanda kwa upande wake pia imekanusha kuhusika na utekaji nyara huo.
Polisi mjini Kampala walimpata Bwana Manirakiza, mwenye umri wa ishirini na mitatu, akiwa hana ufahamu karibu na maeneo ya makaburini, alisema afisa mmoja mwandamizi katika ofisi ya waziri mkuu Douglas Asiimwe.


Ramani ya Congo
''Alikuwa na majeraha mengi na kuvuja damu, pia kulikuwa na ishara kuwa walikuwa ameteswa sana'' Alisema Asiimwe.
Manirakiza kwa sasa anapokea matibabu katika hospitali kuu ya taifa ya Mulago mjini Kampala chini ya Ulinzi mkali.

Afisa huyo wa serikali ya Uganda amesema wanatarajia raia huyo wa Rwanda kupona na kupata ufahamu siku chache zijazo ili kuelezea zaidi wale waliomteka nyara.
Wiki iliyopita, mkimbizi mwingine ambaye Umoja wa Mataifa ulikuwa umeelezea wasi wasi kuhusu hali yake, Joel Mutambazi, ambaye ni afisa wa zamani wa jeshi la Rwanda amewekwa chini ya ulinzi wa ofisi ya rais wa Uganda Yoweri Museveni.

Wakimbizi wadai kutekwa nyara

Awali, Mutambazi alikuwa amekamatwa na maafisa wa polisi baada ya serikali ya Rwanda kutoa idhini ya kukamatwa kwake.
Umoja wa Mataifa ulipinga kukamatwa kwake na kuitaka serikali ya Uganda kutoa hakikishom kwa wakimbizi wote walioko nchini humo.

Polisi wa Uganda

Serikali ya Uganda imekataa ombi la serikali ya Rwanda ya kutaka afisa huyo wa zamani kurejeshwa Nyumbani.

Mmoja wa wakimbizi hao hajulikani aliko.
Mwezi uliopita, Manirakiza aliliambia BBC kuwa alikuwa mwanafunzi nchini Rwanda na alilazimishwa kujiunga na wapiganaji wa waasi wa M23 nchini Congo, lakini alifanikiwa kutoroka na kutafuta hifadhi nchini Uganda.

Umoja wa Mataifa na serikali ya Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo, zimeishutumu Rwanda kwa kuwaunga mkono waasi wa M23, madai ambayo yamepingwa vikali na Rwanda.
Mwaka wa 2010, aliyekuwa mkuu wa majeshi ya Rwanda Faustin Kayumba Nyamwasa alitorokea nchini Afrika Kusini.

Nyamwasa alidai kuwa serikali ya rais Paul Kagame ilikuwa na njama ya kutaka kumuangamiza, baada ya kupigwa risasi na kujeruhiwa mjini Johannesburg.
Share this article :

Post a Comment

 
Copyright © 2011. TANGA LEO - All Rights Reserved
Proudly powered by Blogger