Featured Post Today
print this page
Latest Post

Ameipa Tanzania utajiri, yeye amebaki masikini

Ameipa Tanzania utajiri, yeye amebaki masikini

318_ngoma_1b973.jpg

KILA mwaka, madini aina ya Tanzanite huiingizia Tanzania kiasi cha dola milioni 20 (zaidi ya Sh bilioni 30). Duniani kote, madini hayo hayo huingiza wastani wa dola milioni 500 (zaidi ya Sh bilioni 800).
Wakati mabilioni yote hayo yakiingia mfukoni mwa serikali na wafanyabiashara, mgunduzi wa madini hayo, Jumanne Mhero Ngoma (74), anaishi kwa kutegemea ruzuku za watoto. Mapato yake kwa mwaka ni shilingi za Tanzania sifuri!


Nilikutana na Mzee Ngoma siku chache zilizopita jijini Dar es Salaam katika ofisi ya mmoja wa wanawe. Pamoja na masahibu na mikasa mbalimbali iliyomkumba katika maisha yake, bado aliweza kunipokea kwa bashasha na tabasamu.

Amefanya mahojiano na vyombo mbalimbali vya habari na pengine ameanza kuchoka sasa. Mvi kichwani kwake na kwenye eneo la ndevu ni ishara kwamba umri unaanza kumtupa Mzee Ngoma.
Nimekaa namtazama. Huyu ndiye mtu aliyegundua madini ya Tanzanite. Alipaswa kuwa utambulisho wa Watanzania. Katika nchi nyingine zinazothamini watu wake, huyu alitakiwa kufahamika na watu wote waliomaliza elimu ya msingi.

Kama ambavyo watoto wote wa Kimarekani wanavyomfahamu Thomas Edison (mbunifu mashuhuri na mfanyabiashara wa karne kadhaa zilizopita) . Lakini mbele ya macho yangu, alikaa mzee mmoja ambaye kama ningekutana naye kwenye daladala (na ndiyo usafiri wake mkuu), nisingemtazama mara mbili.

Namuuliza swali moja la msingi kwamba ilikuwaje yeye aliyagundua madini ambayo wakoloni (wazungu) walishindwa kuyabaini kwa muda wote waliokaa hapa nchini.
"Nakumbuka kila kitu kuhusu mara yangu ya kwanza kuona madini hayo. Mara ya kwanza kuyagundua madini haya nilikuwa mdogo sana. Nilikuwa na umri wa chini ya miaka 20 na nilikuwa porini nikichunga mifugo.

"Nilikuwa kwenye msitu ambao Wamasai walikuwa wameupa jina la Lalouo. Eneo ambako niliyaona lilikuwa linafahamika kwa jina la Naisunyai ambako kwa kawaida Wamasai walikuwa wakilitumia kunywesha mifugo yao.

"Siku hiyo niliona vitu vinavyowaka. Nikawa nashangaa vitakuwa ni vitu gani. Awali nilidhani pengine ni nyoka au wanyama wa hatari. Nikasogea nikiwa na upinde na mshale wangu tayari kwa lolote
"Nilipogusa na mti niliokuwa nimeushika, nikashangaa mawe yanayong'aa yakitoka ardhini. Vipande vidogo vidogo vyenye rangi ya bluu. Kwa kweli nilivipenda sana.
"Nilishangaa sana lakini ghafla nikakumbuka kuwa nilikuwa nachunga mifugo. Kumbe ng'ombe na mbuzi niliokuwa nawachunga walikuwa wamekimbia tayari. Nikaacha shughuli hiyo na kwenda kuwafuata.
"Kwa bahati nzuri, nilifuatilia njia walizopita hadi nikawapata wote. Lakini ilikuwa kazi ngumu maana ule ulikuwa msitu mkubwa. Nikarudi nyumbani nikiwa na mifugo ile na nikawa nimesahau kabisa habari za madini yale kwa muda ule," anasema.

Mtoto wa Ngoma aitwaye Asha aliyekuwa mwenyeji wetu kwenye ofisi ile ananiuliza kama naweza kutumia kinywaji chochote. Namwomba samahani kwa kuwatia hasara maana nikaagiza vinywaji viwili badala ya kimoja. Maji na soda. Kwenye dunia hii ya kisukari, kunywa soda pekee bila kuchanganya na maji kunaleta hatari ya kuongeza sukari mwilini.

Mzee Ngoma yeye anaomba maji tu. Tunasubiri kidogo. Tunapiga mafunda mawili matatu na kisha tunaendelea na mazungumzo yetu.
Hata hivyo, mwaka 1966 ilitokea bahati iliyobadilisha maisha yangu. Mwanzoni mwa mwaka huo, serikali ilitangaza kuwepo kwa mafunzo kuhusu utafiti wa madini yaliyopangwa kufanyika mkoani Morogoro.

"Mimi wakati huo nilikuwa nafanya biashara zangu tu lakini nilikuwa mpenzi sana wa masuala ya madini na ndiyo nilipoyaona madini yale ya Tanzanite kwa mara ya kwanza nilishikwa na hamu ya kutaka kuyajua.

"Ulitakiwa kujilipia mwenyewe nauli na gharama nyingine halafu serikali inakulipia mafunzo hayo kwa muda wa wiki tatu. Nikazungumza na mke wangu kuhusu hilo na akaniruhusu niende kwenye mafunzo.

"Nilikwenda Morogoro na hatimaye nikafaulu kwenye mafunzo hayo. Ilipofika tarehe sita, mwezi wa sita mwaka 1966, nikapewa cheti cha utafiti ambacho ninacho hadi leo. Pamoja na mambo mengine, cheti hicho kilikuwa kinakuwezesha kufahamu madini na sifa zake mbalimbali," anasema.

Ni mafunzo hayo ambayo baada ya kuyamaliza yalimfanya Ngoma aweze kugundua madini hayo ya Tanzanite.

Lakini kabla ya madini hayo, mzee huyu kwanza aligundua madini aina ya Gypsum ambayo sasa yanatumika katika nyumba nyingi za Watanzania wenye kipato kuanzia cha kati hadi cha juu.
Aliyagundua madini hayo katika eneo la Chankoko, Makanya mkoani Kilimanjaro.

"Wakati nikigundua madini hayo, hayakuwa na kazi sana. Watu wengi hawakujua kazi yake. Kwa bahati nzuri, katika wakati huohuo, kukawa na kiwanda cha saruji cha WAZO ambacho kilitaka kuanza kufanya shughuli zake na gypsum ilikuwa ni malighafi nzuri sana.

"Kuna bwana mmoja aitwaye Petro Gerson Kizigha akanikutanisha na wazungu waliokuwa wakitaka kuanzisha kampuni hiyo na tayari wakiwa na taarifa za gypsum niliyoigundua.

"Nakumbuka majina ya wazungu hao yalikuwa ni Florench, Carter na Habel. Walikuja hadi Makanya kwa ndege binafsi na walishukia katika shamba la katani la bwana mmoja aliyekuwa akiitwa Hassan.
"Walipoona gypsum ile wakaipenda sana. Wakaagiza mara moja mzigo wa tani 36 ambao tuliupakia kwenye mabehewa. Kuna barabara kutoka Chankoko hadi stesheni ya reli ya Makanya yenye urefu wa kilomita 10 ilijengwa ili kurahisisha usafirishaji wa bidhaa hiyo.

"Mimi ndiye niliyepewa jukumu la ujenzi wa barabara hiyo. Nilipewa na wazungu wale kiasi cha Sh 8,000 kwa ajili hiyo. Kwa wakati huo, hiyo ni hela nyingi sana. Wajenzi walikuwa wakilipwa shilingi nne kwa siku na zilikuwa nyingi kiasi kwamba watu walikuja kuomba kazi kwa wingi hadi wengine nikawakataa, anasema.

Pamoja na mafanikio hayo katika biashara ya gypsum, kuna kitu kimoja kilikuwa kinamsumbua Ngoma kichwani kwake. Yale madini aliyoyaacha kule Umasaini, Marerani yalikuwa ni madini gani?
"Ndipo siku moja nikawachukua ndugu zangu na kuwaomba wanisindikize kwenda kwenye ule msitu wa Lalouo ili nikayachunguze tena yale madini. Niliomba kusindikizwa kwa sababu ule msitu ni mkubwa na nilitaka pia nipate watu wa kunisaidia kubeba.

"Nakumbuka tulichimba karibu kilo sita za madini hayo. Kuna jiwe moja lilikuwa na ukubwa wa takribani gramu 55 hivi. Jiwe kubwa tu. Ndilo lililokuwa kubwa zaidi.

"Nikalipeleka Moshi kwenye Ofisi ya Mkaguzi wa Madini aliyekuwa akiitwa Bills wakati huo. Mzungu huyo. Akayatazama na akasema hajawahi kuona kitu kama kile. Akahisi yanaweza kuwa Blue Tomaline, lakini tukakubaliana kuwa si yenyewe.

"Mimi nikamuuliza sasa mwenzangu unadhani haya ni madini gani? Unajua wazungu ni watu wakweli kidogo. Wana matatizo yao lakini hawapendi kusema uongo. Akasema kwa kweli siyajui. Inabidi tuyapeleke kwenye maabara ya serikali iliyokuwa iko Dodoma.
"Nikampa sampo yote niliyokuwa nayo lakini lile jiwe kubwa zaidi nikabaki nalo. Alipoliona, mke wa bwana Bills akawa amelipenda sana. Akaniomba abaki nalo.

"Nikakataa. Nikamwambia kama nikikupa, nitakuwa nakupa nini? Maana mumeo ambaye ndiye mtaalamu wa mambo haya ameshindwa kuyajua. Siwezi kukupa na nitabaki na hili kama kumbukumbu yangu.

"Ilipofika Septemba 23 mwaka 1967, ndipo nikapokea barua rasmi kutoka maabara ya Dodoma. Vipimo vikaonyesha madini yale yanafahamika kwa jina la Zoisite. Ndiyo maana tunasema madini hayo yaligunduliwa rasmi mwaka huo wa 1967 kwa sababu ndipo cheti kile cha maabara kilipotoka," anasema.

Katika simulizi kuhusu gunduzi mbalimbali za madini hapa nchini, zipo zinazoeleza namna wananchi wa Shinyanga walivyokuwa wakicheza bao kwa kutumia almasi kwa sababu hawakujua thamani yake.

Hali iko hivyo kwa Mzee Ngoma ambaye alikuwa akilitumia jiwe hilo la gramu 55 kwa ajili ya kuzuia karatasi zake zisipepee kutoka mezani kwake. Lilikuwa jiwe la kawaida kabisa ndani ya nyumba yake.

Nimeangalia bei ya sasa ya Tanzanite ili upate picha ya nini mzee huyu alikuwa nacho ndani kwake. Kwa sasa, bei ya madini hayo katika soko la dunia inacheza kati ya dola 500 hadi 700 kwa karati moja.

Zipo taarifa kwamba zipo sehemu duniani ambako watu wanauziwa hadi dola 1000 kwa karati moja. Tuseme wastani ni dola 600 (sh 800,000) kwa karati moja.

Karati moja ni sawa na gramu 0.2. Gramu 55 maana yake ni karati 275. Kama bei ya karati moja ni Sh 800,000, bei ya karati 275 ni sawa na takribani Sh milioni 220.

Mzee Ngoma alikuwa anatumia Sh milioni 220 kuzuia karatasi na magazeti yasipeperuke kutoka mezani kwake ! Mzee huyu hakujua kitu wakati huo.

Jiwe hilo kipenzi la mgunduzi huyu likaja kumpotea katika mazingira ya kutatanisha. Simulizi yake, ilinifanya niombe mahojiano haya yapumzike kidogo ili niweze kuvuta pumzi.
"Nilikuwa na marafiki wawili wenye asili ya kihindi waliokuwa wakiishi Handeni mkoani Tanga. Mmoja akiitwa Habib Esack Ismail na mwingine akijulikana kwa jina la Nuru Skanda. Walikuja siku moja nyumbani kwangu na wakaliona lile jiwe.

"Wakaniomba waende nalo kwao (Handeni) ili wakawaonyeshe wazazi wao wajue la kufanya. Wakati huo, Zoisite ama Tanzanite kama inavyofahamika sasa, haikuwa maarufu sana na matumizi yake hayakuwa yakijulikana.

"Walisema watalirudisha baada ya siku tatu. Nikawapa na wakaondoka nalo. Hawakurudi baada ya siku tatu na sijawaona tena tangu wakati huo. Siku moja nilikutana na aliyekuja kuwa Kamishina wa Madini hapa nchini aliyejulikana kwa jina la Luwena na akaniambia lile jiwe liko Ujerumani na waliuziwa kwa Sh 6000 kwenye miaka hiyo.

"Hizo ni hela nyingi sana. Ina maana akina Habib waliliuza na wakaondoka zao. Lile jiwe linaniuma sana maana kama ningebaki nalo pengine lingeweza kunipa fedha nyingi," anasema Ngoma.
Machungu ya Mzee huyu hayakuishia hapo. Kuna unyama mwingine mkubwa zaidi ambao alifanyiwa.

Baada ya kuibiwa jiwe lake hilo, akili ya Ngoma ilifanya kazi haraka na akaamua kwenda kupata leseni ya umiliki wa eneo ambako aliyapata madini yale.

Akapewa viwanja nane kwenye eneo lile la Lalouo ambako alilipia kiasi cha Sh 15 kwa kila kimoja. Akaweka alama zote muhimu na kuamini kwamba lile ni eneo lake halali kisheria na mara wakati utakapofika, ataanza kuchimba madini hayo.
"Siku moja mwezi Februari mwaka 1968, nikaenda kutembelea kwenye eneo lile. Nikamkuta kijana mmoja anaitwa Daudi Mayaya akiwa anachimba madini hayo kwenye eneo langu. Alikuwa ameyajaza kwenye ndoo.

"Nikamwambia kwanini amechimba madini hayo kwenye eneo langu? Akanijibu kwamba lile si eneo langu bali ni la mtu mmoja aiwaye De Souza (Huyu nitamweleza zaidi baadaye). Nikamwonyesha alama zangu zote nilizoweka pamoja na nyaraka nilizokuwa nazo.

"Nilipoenda kushitaki Polisi kuhusu huyu mtu anayeitwa De Souza, nikaambiwa ataitwa na atafika Jumatatu. Bila ya taarifa, kumbe huyo bwana akaja Jumamosi na akazungumza na polisi mapema.
"Mkuu wa Polisi kwenye eneo letu alikuwa akifahamika kwa jina la Herbert Kitenge. Huyu bwana akaniita Polisi na akaniambia ameamua kumpa De Souza vitalu (viwanja) vinne kati ya nane nilivyokuwa navimiliki.

"Sasa mimi nikabaki nimeshangaa, inakuaje mtu anapewa vitalu vyangu. Lakini afande Kitenge akasema ama nikubali hiyo dili au nitanyang'anywa vyote. Nikakasirika sana na nikasusa kabisa. Sikurudi tena kule kwenye machimbo. Nikaenda kufanya biashara zangu," anasema kwa huzuni.

Mzee Ngoma anamtaja De Souza mara nyingi katika maelezo yake. Manuel De Souza, mzaliwa wa Goa nchini India alikuja nchini Tanganyika mnamo mwaka 1933 akiwa na umri wa miaka 20 tu na tayari akiwa fundi cherehani mzuri.

Taarifa katika mitandao mbalimbali duniani inamtaja yeye kama mvumbuzi wa Tanzanite. Mtandao wa Ilios Jewellers unadai kwamba Julai mwaka 1967, kundi la Wamasai, lilimpeleka Mhindi huyo kwenye eneo ambako aligundua madini hayo.

Kwenye mtandao unaoheshimika zaidi duniani wa Wikipedia unamtaja fundi cherehani, Emmanuel Merishiek Mollel kama mgunduzi wa madini hayo. Katika maelezo yake, mtandao huo unadai kwamba ni Mollel ndiye aliyempa De Souza madini hayo na yeye akayapeleka kwa wataalamu ambao waliyabaini kwamba ni Tanzanite.

Hata historia inapindishwa ili Mzee Ngoma akose hadhi na heshima anayostahili !
Kabla ya kuitwa Tanzanite, madini haya yalikuwa yakifahamika kwa jina la Zoisite. Jina hilo, kwa mujibu wa maelezo ya nyaraka mbalimbali, lilitokana na raia wa Austria, Siegmund Zois, ambaye alikuwa akifadhili safari mbalimbali za watu waliokuwa wakitafuta madini mbalimbali.

Kwa Kijerumani, neno Zoisite linafanana kimatamshi na neno la Kiingereza Suicide. Kampuni iliyokuwa ikifanya biashara ya Tanzanite ya Tiffany& Co. ndiyo ikaamua kubadili jina hilo na kuyaita madini hayo Tanzanite ili liwe na mvuto.

Hakukuwa hata na mmoja aliyeona yanafaa kuitwa Ngomanite au Ngomasite !
Mwaka 1984, serikali iliamka kutoka usingizini na kumtaja Mzee Ngoma kama mvumbuzi wa madini hayo. Kama zawadi yake kwa uvumbuzi huo wa kihistoria, serikali ilimpa mzee huyo Ngao, cheti cha kumtangaza kama mvumbuzi na fedha taslim Sh elfu 50,000.
Kwa mujibu wa Wikipedia, katika kipindi cha kati ya mwaka 1967 hadi mwaka 1972 wakati serikali ilipoamua kutaifisha shughuli za uchimbaji wa Tanzanite, kiasi cha karati milioni mbili zilikuwa tayari zimechimbwa kutoka Mirerani.

Kwa bei ya sasa ya karati moja, maana yake ni kwamba kwa miaka hiyo mitano pekee, De Souza, washirika wake kama vile Ally Juyawandu na askari jeshi mmoja aliyekuwa na asili ya Ugiriki aliyefahamika kwa jina moja tu la Papanichalou, walifanikisha biashara yenye thamani ya takribani Sh trilioni 1.6 kwa thamani ya sasa !

Watoto wa De Souza aliyefariki dunia mwaka 1969 akiwa na umri wa miaka 56 kwa ajali ya gari, wametapakaa katika nchi mbalimbali kama vile Denmark, Malta na Uingereza, pengine wakila faida ya 'ugunduzi' wa baba yao.

Kwa upande mwingine, Mzee Ngoma amejibanza katika ofisi ndogo ya mwanaye Asha katikati ya jiji. Fedha pekee ambayo ameitengeneza kutokana na kuipa Tanzania sifa na utajiri huu wa kipekee ni Sh elfu 50,000 zile alizopewa na Hayati Rashid Mfaume Kawawa !
Namuuliza shujaa huyu wa taifa anataka nini kutoka kwa serikali; "Sihitaji mambo makubwa sana. Ninachohitaji ni kuishi maisha yanayofanana na Tanzanite. Nataka mtu akiniona mimi aone Tanzanite," anasema.

Ni ombi ambalo linanisisimua. Watanzania wanapaswa kuwafahamu watu kama akina Ngoma. Serikali inapaswa kuwaenzi watu kama akina Mzee Ngoma.

Hawa watachochea watu wawe wagunduzi zaidi. Simulizi zao zitafanya watu wajenge akili ya kuhoji kila wanachokiona. Nani ajuaye, pengine kuna 'Tanzanite' nyingine katika maeneo mbalimbali hapa nchini lakini hazijulikani kwa vile hakuna akina Ngoma?

Nani atataka kuwa mgunduzi wa vitu vya thamani iwapo wagunduzi waliopo tunapanda nao daladala, tunashinda nao njaa na hawathaminiki?

Serikali imfanye Mzee Ngoma afanane na faida ambayo Tanzanite imeiletea nchi yetu.


0 comments

Jaji mkuu akamatwa kwa rushwa Indonesia

Jaji mkuu akamatwa kwa rushwa Indonesia

indonesia_akil_mochtar_304x171_afp_nocredit_ab639.jpg

Jaji mkuu wa mahakama ya kikatiba nchini Indonesia amekamatwa kwa madai ya rushwa.
Akil Mochtar alikamatwa na maafisa wa kupambana na rushwa kwa madai ya kupokea dola laki mbili na nusu kama rushwa.

Kwa mujibu wa maafisa hao, kukamatwa kwa Mochtar ni tukio la kwanza la hivi karibuni kukamatwa kwa afisaa mkuu wa umma kuhusiana na rushwa aliyopokea akisikiliza kesi kuhusu uchaguzi.

Mahakama ya kikatiba ya Indonesia husikiliza kesi zote kuhusiana na uchaguzi.
Bwana Mochtar alichaguliwa mwaka huu kwa muhula wa miaka mitano kwa wadhifa huo katika mahakama ya kikatiba.

Alikamatwa kwake nyumbani mjini Jakarta baada ya mfanyabiashara ambaye pia ni mbunge kumkabidhi pesa, kwa mujibu wa msemaji wa tume ya kupambana na rushwa nchini humo.
Kesi hiyo ilihusishwa na utata ulioibuka katika uchaguzi uliofanyika kisiwani Borneo.
Watu wengine wawili wamekamatwa baada ya kuhusishwa na kesi hiyo.
Mwezi jana mahakama ya kupambana na rushwa ilimpata na hatia generali wa polisi Djoko Susilo kwa kosa la kutengeza pesa haramu.

Susilo alihukumiwa jela kifungo cha miaka 10 na kutozwa faini.
0 comments
 
Copyright © 2011. TANGA LEO - All Rights Reserved
Proudly powered by Blogger