Featured Post Today
print this page
Latest Post

Habari zilizotufikia hivi punde zinasema Mtangazaji Julius Nyaisanga amefariki Dunia mkoani Morogoro

Habari zilizotufikia hivi punde zinasema Mtangazaji Julius Nyaisanga amefariki Dunia mkoani Morogoro

Taarifa za kushtua katika tasnia ya habari na utangazaji kutokana na habari za kifo cha Mtangazaji mkongwe nchini Tanzania, Julius Nyaisanga, aliyekuwa mfanyakazi wa Abood Media mjini Morogoro.
 Julius Nyaisanga

 Kaimu Meneja wa Abood Media Abeid Dogoli ameithibitishia blog hii kwamba ni kweli mtangazaji wa siku nyingi Tanzania Julius Nyaisanga amefariki dunia leo asubuhi.

Amesema Nyaisanga alipelekwa hospitali ya Mazimbu Morogoro jana saa nane mchana kutokana na kusumbuliwa na Kisukari pamoja na presha ambapo asubuhi ya leo October 20 2013 ndio akafariki dunia akiwa na umri wa miaka 53.

Mara yake ya mwisho kuingia ofisini ilikua juzi japo alikua ameanza likizo toka October 12 ambapo huu ulikua ni mwaka wake wa tatu toka ameanza kufanya kazi na Abood Media ya Morogoro kama Meneja wa kituo.

 Katikati ni Julius Nyaisanga akiwa na wadau wengine wa habari. Kushoto ni Abubakar Lyiongo na kulia ni Othman Michuzi.
 
0 comments

Edo Kumwembe: Sikuwa na mkataba Coastal Union

Edo Kumwembe: Sikuwa na mkataba Coastal Union


Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam

MSEMAJI wa zamani wa Coastal Union, Edo Kumwembe, amesema kwamba hakuwa na mkataba wowote ndani ya timu hiyo yenye maskani yake jijini Tanga, badala yake alikuwa akifanya kazi kwa kujitolea kama mdau wa mpira wa miguu.

Edo Kumwembe, pichani.

Kumwembe aliyasema hayo siku chache baada ya kudaiwa kuwa amemaliza mkataba wake ndani ya timu hiyo na hakuna juhudi za kuongeza ili aendelee na kibarua chake.


Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Kumwembe ambaye pia ni mchambuzi wa mambo ya soka, alisema kuwa lolote linalotokea ndani ya timu hiyo hawezi kulalamika kwakuwa tangu mwanzo hakuwa na mkataba wowote.


Alisema jambo hilo linamfanya aone kuwa hana anachoharibikiwa katika suala hilo, ambalo habari zinazotolewa katika vyombo vya habari zinasema Kumwembe na kocha wa Coastal Union, Hemed Morocco mikataba yao imekwisha.


“Kama unazungumzia kocha wa Coastal Union sawa, ila kwa upande wangu sikuwa na mkataba wa kuwa msemaji wa timu hiyo yenye maskani yake jijini Tanga kwa wagosi wa kaya,” alisema.


Aidha, Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Klabu ya Coastal Union ya Tanga, Albert Clement Peter , maarufu kama ‘Mkubwa wa Kazi’ alikanusha vikali taarifa zilizosambazwa na baadhi vyombo vya habari kuwa wamemfukuza kocha wao Morocco.


“Hatujamfukuza kocha huyo kama ilivyoripotiwa bali mkataba wake wa kuendelea kuinoa timu hiyo umekwisha hivyo tutaandalia hatima yake, huku kwa sasa akiwa Bukoba kwa ajili ya kukipiga na Kagera Sugar ya mjini humo,” alisema.


Kwa mujibu wa Peter, uongozi unakaa kuangalia namna gani ya kuendelea na kocha huyo au wamuache, ila si kweli kuwa tayari ameshaondolewa kikosini.
0 comments

MATUKIO YA MAAFALI YA KWANZA YA SHULE YA SEKONDARI ELOHIM YA JIJINI TANGA.

MATUKIO YA MAAFALI YA KWANZA YA SHULE YA SEKONDARI ELOHIM YA JIJINI TANGA.

MKUU WA WILAYA YA TANGA,HALIMA DENDEGO KULIA AKIPATA MAELEKEZO KUTOKA KWA WANAFUNZI WA SHULE YA SEKONDARI ELOHIM LEO.


MKURUGENZI WA SHULE YA SEKONDARI ELOHIM YA TANGA,ELINGAYA MUNGURE AKIZUNGUMZA WAKATI WA MAHAFALI HAYO.

WANAFUNZI WANAOHITIMU WAKISAKATA LUMBA .

MKUU WA WILAYA YA TANGA,HALIMA DENDEGO AKIONGOZA HARAMBEE KWENYE SHULE HIYO

MKUU WA WILAYA YA TANGA,HALIMA DENDEGO ALIZUNGUMZA WAKATI AKITOA HOTUBA YAKE KWENYE MAHAFALI HAYO LEO

WANAFUNZI WANAOMALIZA WAKIIMBA WIMBO WA TAIFA LEO HII





Na Lodrik Nowi, Tanga.

Mkuu wa wilaya ya tanga Bi.halima dendegu ametoa agizo kwa mkurugenzi mtendaji kuhakikisha kuwa ndani ya siku kumi na nne barabara itokayo chalinze tanga kuelekea shule ya sekondari ya Heloim iwe imetengenezwa kwa kiwango kizuri.
Agizo amelitoa wakati akiweka jiwe la msingi iliyokwenda sambamba na  mahafali ya kwanza ya kidato cha nne yaliyofanyika katika shule ya sekondari ya heloim.
Mbali na kutoa agizo hilo Dendegu ameahidi kutoa vitanda nane kwa ajili ya wanafunzi wa shule hiyo ili kuweza kuboresha mazingira mazuri kwa wanafunzi na  kuongeza kiwango cha ufaulu.
Kwa upande wao wazazi wa watoto wanaosoma ktk shule hiyo wamechangia fedha kwaajili ya vitanda viwili, na kuhaidi kuendelea kutoa ushirikiano wa hari na mali kwa uongozi wa shule hiyo.
Kwa upande wake mkuu wa shule hiyo Bw.geofrey  makanza amesema kuwa changamoto inayowasumbua ni wazazi kutolipa ada kwa wakati pamoja na baadhi ya wanafunzi kutojitambua kitaaluma.
Aidha mkurugenzi wa shule hiyo Bi.Elingaya Mungure ameiomba serikali iweze kushirikiana na shule hiyo shule bega kwa bega ili kufikia malengo ya elimu bora kwa kila mtanzania.









0 comments

MSHAHARA WA RAIS KAA LA MOTO..SEREKALI YASEMA ZITTO ALIKOSEA KUTAJA MSHAHARA WA MTU

MSHAHARA WA RAIS KAA LA MOTO..SEREKALI YASEMA ZITTO ALIKOSEA KUTAJA MSHAHARA WA MTU

Dar es Salaam. Siku chache baada ya Mwenyekiti wa Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC), Zitto Kabwe kutaja hadharani mishahara ya Rais Kikwete na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, serikali imekataa kuizungumzia mishahara hiyo.

Msimamo wa Serikali kutotaja mishahara ya viongozi wakuu unatofautiana na utamaduni wa nchi nyingine kama Marekani, Afrika Kusini, Ufaransa na Kenya ambazo mishahara ya wakuu wake huwekwa wazi kwa umma.

Zitto ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa Chadema akiwa wilayani Igunga Mkoani Tabora, alisema Rais Kikwete anapokea zaidi ya Sh30 milioni kwa mwezi (sawa na Sh360 milioni kwa mwaka) ikiwa ni marupuru na mshahara kwa mwezi bila kodi, huku Pinda akipokea Sh 26 milioni kwa mwezi.

Akizungumza na Mwananchi kwa simu jana, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Celina Kombani alisema kiongozi yeyote haruhusiwi kutaja mshahara wa mtu mwingine kwa kuwa kufanya hivyo ni kinyume cha sheria ya utumishi wa umma.

“Kuutaja mshahara wa mtu mwingine ni kinyume cha sheria na kosa, siyo utaratibu. Kwani wewe upo tayari watu waujue mshahara wako?” alihoji.

Aliongeza kuwa ingawa mishahara ya viongozi hao inatokana na kodi za wananchi, sheria ndiyo inayozuia watu kuyataja malipo hayo hadharani na kwamba hayupo tayari kuutaja mshahara wa rais au kiongozi mwingine labda mtu huyo autaje yeye mwenyewe.

“Siwezi kutaja mshahara wa bosi wangu wala wa kwangu mwenyewe. Wewe unaujua mshahara wa Obama (Rais wa Marekani)?” alihoji tena.

Akizungumzia mishahara ya marais wa nchi nyingine duniani kuwekwa wazi, Kombani alisema kila nchi ina utaratibu wake na kwamba Tanzania haijafikia hatua hiyo.

Alipotafutwa kulizungumzia suala hilo, Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue simu yake ya mkononi iliita bila kupokewa. Gazeti hili pia liliwasiliana na Naibu Mtendaji Mkuu mwenye jukumu la kuanzisha na kuongoza Idara ya Mageuzi ya Kilimo Ofisi ya Rais Ikulu, Peniel Lyimo ambaye alisema yeye si mhusika. “Masuala yote yanayohusu utumishi yapo Wizara ya Utumishi,” alisema Lyimo.

Akianika mshahara wa Waziri Mkuu, Zitto alisema kwamba kiongozi huyo analipwa Sh11.2 milioni kama mbunge, Sh8 milioni kama waziri na Sh7 milioni kwa nafasi yake ya Waziri Mkuu, hivyo, kumfanya kupokea zaidi ya Sh300 milioni kwa mwaka.

Hata hivyo, Kombani alilionya gazeti hili kuandika taarifa za mishahara ya watu kwa kuwa kufanya hivyo ni kosa.


Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Bashiru Ally alisema Mwalimu Nyerere aliwahi kutaja mshahara wake hadharani na kuhoji viongozi wanaotaka mishahara yao isitajwe wanaficha nini


“Hata wakificha mishahara yao bado wananchi wataona maisha wanayoishi kuwa si safi,” alisema.



Wanaharakati pia wahoji

Mwenyekiti wa Jukwaa la Katiba Tanzania (Jukata), Deus Kibamba alisema siyo kosa kwa mtu yeyote kutangaza mshahara wa viongozi wa umma kwa kuwa wanalipwa kutokana na kodi za wananchi.

Aliongeza kuwa kuanzisa sasa atakuwa balozi wa kutangaza mishahara ya viongozi hao, ili kila mwananchi aweze kufahamu kama ambavyo imekuwa ikifanyika katika nchi nyingine duniani.

“Ninachojua mimi ni kuwa dhana ya mshahara inataka kuwepo na siri baina ya mwajiri na mwajiriwa, lakini si kwa viongozi wa umma ambao wanalipwa na kodi za wananchi. Kuanzia sasa hivi nitakuwa balozi wa kutangaza mishahara ya viongozi hao ili kila mtu ajue,” alisema Kibamba.

Katibu Mkuu wa Tanzania Labor Party (TLP), Jeremiah Shelukindo alisema ni vyema kila mtu akaheshimu sheria inayozuia kutaja mshahara wa mtu mwingine kwa kuwa kitendo hicho kinaweza kuwaudhi baadhi ya viongozi wa umma.

“Si vizuri kuingiza siasa kwenye mambo ya mishahara. Siyo mara ya kwanza kusikia watu wakijaribu kutaja mishahara ya watu wengine huko ni kukiuka sheria,” alisema.

Naye Mkurugenzi wa asasi ya Sikika, Irenei Kiria alisema umefika wakati ambapo inabidi uanze kufanyika mchakato wa kuzibadili sheria zinazolenga kulinda masilahi ya viongozi wa umma.


“Tunataka kujua viongozi wanalipwa shilingi ngapi na kwa nini wanalipwa kiasi hicho,” alisema Kiria.


Nchini Marekani, mshahara wa rais unajulikana tangu mwaka 1789 kiongozi wa nchi hiyo alipokuwa analipwa Dola 25,000 kwa mwaka.

Kuanzia 2001 hadi sasa, Rais wa Marekani analipwa Dola 400,000 (Sh 640 milioni) kwa mwaka, sawa na Sh 53.3 milioni kwa mwezi.

Rais wa Afrika Kusini, Jacob Zuma analipwa Randi 2 ,917 038 sawa na zaidi ya Sh400 milioni za Kitanzania kwa mwaka, Rais wa Ufaransa, Francois Hollande Sh475 milioni, Waziri Mkuu wa Uingereza, David Cameron Sh338 milioni, Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya Sh277 milioni na Rais wa Namibia, Hifikepunye Pohamba Sh226 milioni kwa mwaka.

Wengine na malipo wanayopata kwa mwaka ni Marais wa Urusi, Vladimir Putin, Sh174 milioni, Ellen Johnson Sirleaf wa Liberia Sh137 milioni, Michael Satta wa Zambia, Sh126 milioni, Rais wa Angola, Jose dos Santos Sh91 milioni, Rais wa Lesotho, Profesa Pakalitha Mosisili Sh88 milioni, Armando Guebuza wa Msumbiji, Sh84 milioni na Rais wa Jamhuri ya Watu wa China, Xi Jinping Sh60 milioni.


Wengine ni Rais wa India, Pranab Mukherjee Sh49 milioni, Rais wa Zimbabwe, Robert Mugabe Sh27 milioni, Naibu Rais wa Afrika Kusini, Kgalema Mothlanthe Sh331 milioni, Waziri Mkuu wa Namibia, Nahas Angula Sh160 milioni, huku Baba Mtakatifu wa Kanisa la Romani Catholic, Papa Benedict XVI akifanya kazi bila kulipwa mshahara.

Udaku Specially Blog
0 comments

CLUB ZA USIKU, MAMBO HUWA HIVI POMBE NA MZIKI VINAPOKOLEA

CLUB ZA USIKU, MAMBO HUWA HIVI POMBE NA MZIKI VINAPOKOLEA

 Haya ndio Mambo ya Clubs Mziki na Pombe vinapokolewa ...Wengi hujikuta wanasaula kabisa kama picha zinavyoonyesha hapo juu na chini ...Je wewe Umeshawahi Shuhudia Vimbwanga kama hivi ukiwa club?
Udaku Specially Blog
0 comments

Rais Kikwete asimikwa uchifu wa kabila la Wabena wa Njombe

Rais Kikwete asimikwa uchifu wa kabila la Wabena wa Njombe

8607729_orig_9e4fa.jpg
Rais Jakaya Kikwete akipokea Mkuki wakati akisimikwa Uchifu wa Kabila la Wabena na mmoja wa wawakilishi wa Wazee wa Kabila hilo,kwenye wa Hafla ya Uzinduzi wa Mkoa wa Mpya wa Njombe.
n2_35c54.jpg
Wazee wa Kabila la Wabena wakimsimika Uchifu Rais Jakaya Kikwete.
n5_dd1ed.jpg
Chifu Mpya wa Kabila la Wabena, Rais Jakaya Kikwete akiwahutubia wakazi wa Mkoa Mpya wa Njombe.
n6_90b96.jpg
Chifu Mpya wa Kabila la Wabena,Rais Jakaya Kikwete akiteremka Jukwaani baada ya kusimikwa Uchifu wa Kabila hilo na kuwahutubia wananchi wa Mkoa wa Njombe.(P.T)
n9_501e1.jpg
Rais Jakaya Kikwete akipongezwa na Mkewe Mama Salma Kikwete baada ya kusimikwa Uchifu wa Kabila la Wabena,wakati wa Hafla ya Uzinduzi wa Mkoa wa Mpya wa Njombe.
n8_66769.jpg
Pongezi zikiendelea.
n7_5d08e.jpg
Machifu wa Kabila la Wabena wakiwa kwenye picha ya Pamoja.
0 comments

Kenyatta aruhusiwa kutohudhuria baadhi ya vikao vya kesi

Kenyatta aruhusiwa kutohudhuria baadhi ya vikao vya kesi

017113680_35400_1b04e.jpg
Mahakama ya ICC jana Ijumaa(18.10.2013)ilimruhusu kwa kiasi fulani Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta kutohudhuria baadhi ya vikao vya kesi dhidi yake, ili kumpa muda wa kushughulikia majukumu ya kisiasa.
Kenyatta , ambaye alichaguliwa kuwa rais mwezi Machi mwaka huu, amekuwa akidai kwa muda mrefu sasa kuwa kesi hiyo mjini The Hague itazuwia uwezo wake wa kuiongoza nchi.
"Mahakama hiyo kimsingi inamuondolea Uhuru Kenyatta ulazima wa kuwapo wakati wote katika kesi dhidi yake inayoanza Novemba 12, imesema mahakama hiyo ya ICC katika taarifa, lakini ikasisitiza kuwa ni lazima afike kwa ajili ya ufunguzi wa kesi hiyo
Majaji wamesema kuwa ruhusa ya Kenyatta inatolewa kwa misingi kwamba anaweze kutimiza majukumu aliyonayo kama rais wa Kenya, na sio kwasababu ya kutoa hadhi kwa kazi yake kama rais.
Atakuwapo wakati wa kutoa ushahidi
Mahakama hiyo iliyoko nchini Uholanzi pia inasisitiza kuwa Kenyatta anapaswa kuwapo wakati pande zote zitakapokuwa zinatoa taarifa zao za mwisho katika kesi hiyo, wakati wahanga wanatoa ushahidi wao na pia,iwapo kutakuwa na haja wakati wa kikao cha kutoa hukumu.
Kenyatta na makamu wake William Ruto wote wameshtakiwa na mahakama ya ICC kwa madai ya kupanga njama ya ghasia za kikabila ambazo zilisababisha kiasi watu 1,100 kuuwawa na zaidi ya watu laki sita kuachwa bila makaazi baada ya uchaguzi ambao uliingia katika mvutano mwaka 2007.
Kenyatta anakabiliwa na mashtaka matano ya uhalifu dhidi ya ubinadamu ikiwa ni pamoja na mauaji, ubakaji na kuwahamisha watu kwa nguvu kutokana na madai ya kuhusika kwake katika ghasia hizo. Atakuwa rais wa kwanza aliye madarakani kukabiliana na majaji wa ICC.
Ruhusa yasitishwa
Ruto, ambaye kesi yake ilianza mwezi uliopita , alipewa ruhusa kama hiyo akipewa nafasi kutokuwepo mahakamani kwa nyakati fulani , lakini uamuzi huo ulikatiwa rufaa na anatakiwa kuhudhuria vikao vyote hadi uamuzi kuhusu pingamizi iliyowekwa ya rufaa itakapoamuliwa.
Pia mwezi uliopita , mahakama ya ICC, ambayo ni mahakama pekee ya kudumu ya kuhukumu uhalifu mbaya kabisa duniani, ilikataa ombi la wakili wa Kenyatta kutaka kesi yake iahirishwe.
Wakifafanua kuhusu uamuzi huo , majaji wamesema mawakili wa Kenyatta walipewa muda wa kutosha kujitayarisha. Lakini tukio la siku nne za kuzingirwa kwa jengo la maduka ya kifahari mjini Nairobi la Westgate, ambapo watu 67 walipoteza maisha mwezi Septemba , limerejesha hali ya kuungalia uogozi wa Kenyatta na kufika kwake mbele ya mahakama hiyo ya ICC.
Ruto aliruhusiwa kwa muda kutohudhuria kesi dhidi yake ili kusaidia katika kushughulikia mzozo huo.
Wadadisi wa masuala ya kisiasa wanasema kuwa Kenyatta hivi sasa yuko katika nafasi imara zaidi kudai kuwa yeye anapaswa kutoa uhakika kwa umoja wa Wakenya na kwa hiyo nchi hiyo inahitaji uongozi wake.
Aahidi kushirikiana na mahakama
Kenyatta pamoja na Ruto wamesema kuwa watashirikiana na mahakama hiyo, lakini rais hivi karibuni ameishutumu mahakama hiyo katika mkutano wa mataifa ya Afrika kuwa ni chombo cha "mabeberu na wabaguzi wa rangi".
Mjini Nairobi , mmoja kati ya washauri wa kisiasa wa rais Kenyatta jana Ijumaa(18.10.2013) amesema kuwa rais "ataendelea kutoa ushirikiano kwa mahakama ya ICC".
"Wakati nikizungumzia ushirikiano, ina maana ya mambo mengi," amesema Joshua Kutuny. "Lakini nataka kusema kuwa tutaendelea kutoa ushirikiano nao, (akiwa na maana ya ICC ) kwasababu ni ahadi tuliyoitoa wakati wa kampeni yetu wakati wa uchaguzi.
0 comments

KUNA UGUMU GANI SIMBA NA YANGA KUCHEZESHWA NA MAREFA WA KIGENI?

KUNA UGUMU GANI SIMBA NA YANGA KUCHEZESHWA NA MAREFA WA KIGENI?

refa_c932e.jpg
WAKATI leo nyasi za Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam zinatarajiwa kuwaka moto kwa mpambano mkali wa watani wa jadi, Simba na Yanga katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, tayari mizengwe imekwishaanza kuibuka kuhusu marefa.
Yanga SC wanadai hawana imani na refa Israel Mujuni Nkongo, kwa madai aliwahi kuwaonea katika mechi dhidi ya Azam FC msimu uliopita.
Nakumbuka, wachambuzi na watangazaji wa SuperSport waliwahi kuiingiza mechi ya Simba na Yanga katika orodha ya mechi tatu kali za wapinzani wa jadi Afrika - nyingine zikiwa ni kati ya Orlando Pirates na Kaizer Chiefs za Afrika Kusini na Al Ahly dhidi ya Zamalek za Misri.

Lakini mimi naongeza mechi ya wapinzani wa Ghana, Hearts Of Oak na Asante Kotoko, ingawa Kenya nako upinzani wa Gor Mahia na AFC Leopard umeanza kuja juu tena, baada ya kuporomoka miaka ya karibuni, kutokana na kuyumba kwa timu zenyewe.
Hakuna ubishi upinzani wa Ahly na Zamalek huo ni dunia nzima - ni zaidi ya upinzani, lakini kwa Afrika fuatilia ligi nyingi, utagundua Simba na Yanga ni mechi yenye mvuto wa kipekee na ndiyo maana hivi sasa SuperSport wamekuwa wakionyesha mfululizo mechi za watani hao, ingawa hawana mkataba na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) wa kuonyesha mechi za Ligi Kuu.
Unaweza kutilia shaka kiwango cha soka cha timu hizo, lakini si upinzani wao kwa maana ya upinzani. Upinzani wao ni sehemu ya burudani na kama iko siku zitakuwa imara na kucheza soka ya kuvutia, basi burudani itakuwa mara mbili.
Hata hivyo kuna mambo mawili au matatu ambayo kwa kiasi fulani yamekuwa yakipunguza ladha ya mechi za watani hao wa jadi.
Awali tatizo kubwa lilikuwa Uwanja mdogo wa Uhuru, lakini tangu kukamilika kwa Uwanja wa Taifa ambao tumeshuhudia mechi zote zilizochezwa hapo, haijatokea mechi hata moja mashabiki wakajaza viti, mambo yamekuwa mazuri.
Matatizo mawili yaliyobakia ni viwango vya timu kuboreshwa, ili ifike wakati pamoja na upinzani, kukamiana lakini watazamaji washuhudie soka safi.
Tatizo la pili ni marefa, kweli ilipofikia na kama kweli lengo ni kuiongezea msisimko zaidi mechi ya watani, waamuzi wa Tanzania wawekwe kando na watumike waamuzi kutoka nje ya nchi, tena ikibidi nje kabisa ya nchi tatu za Jumuiya yetu ya Afrika Mashariki.
Rejea mchezo wa kufunga pazia la Ligi Kuu msimu wa 2011/2012, Mei 6, 2012, refa alitoa penalti tatu na kadi moja nyekundu kwa Yanga, ikichapwa 5-0 na Simba.
Hii si sahihi katika mechi za wapinzani wa jadi, dhahiri refa huyu alishindwa kuumudu mchezo wa watani hata kama alifuata sheria 17. Katika mechi ya wapinzani wa jadi, ukishatoa kadi moja nyekundu kwa timu moja, unajifikiria sana kurudia kutoa kadi ya pili kwa timu hiyo hiyo.
Katika mechi za wapinzani wa jadi, ukishatoa penalti moja kwa timu moja, unajifikiria sana kutoa penalti ya pili kwa timu hiyo hiyo. Unafikiria mengi. Tena mengi sana.
Haya ni mambo ambayo umefika wakati sasa, TFF wanapoingia kwenye mechi ya watani, wanatakiwa kuyafikiria.
Rejea mechi ya Machi 5, mwaka 2011 Uwanja wa Taifa, refa Orden Mbaga aliivuruga mno mechi hiyo, kutokana tu na pengine mchecheto ama kutaka kufanya kile ambacho kinaitwa 'kubalansi' mchezo au kukwepa lawama, matokeo yake anafanya madudu.
Dakika ya 58 Juma Said Nyosso alimkwatua Davies Robby Mwape kwenye eneo la hatari akawapa penalti Yanga na kilichofuatia wengi walijua beki huyo wa Simba atatolewa nje kwa kadi nyekundu, badala yake akampa kadi ya njano.
Ngumu kuamini Mbaga, refa mwenye beji ya Shrikisho la Soka la Kimataifa (FIFA) hajui alipaswa kufanya nini kwa Nyosso, lakini kwa sababu ni refa wa nyumbani na aliongoza wapinzani wa jadi katika mechi ya nyumbani, alihofia kumtoa mchezaji kwa kadi nyekundu angeshushiwa lawama nzito. Marefa hufanyiwa fujo na kupigwa na mashabiki, labda alihofia hali hiyo pia.
Dakika ya 73 Simba walipata bao safi la kusawazisha lililofungwa kwa kichwa na Mussa Hassan Mgosi, aliyeuwahi mpira uliotemwa na kipa Yaw Berko kufuatia shuti la mpira wa adhabu, lililogonga mwamba wa juu na kudondokea nyavuni kabla ya kuokolewa na mabeki wa Yanga.
Halikuwa bao lenye shaka yoyote, hakukuwa na kuotea wala dosari yoyote, lakini haieleweki kwa nini Mbaga alilikataa bao hilo awali.
Ilikuwa offside au mpira haukutinga nyavuni hadi akalikataa kwanza? Haijulikani, lakini alilikubali baada ya wachezaji wa Simba kumuambia aangalie kwenye TV iliyokuwapo uwanjani marudio ya tukio lile na baada ya hapo akaenda kujadiliana na msaidizi wake, ndipo akalikubali.
Mbaga alichemsha- lakini si Mbaga tu, marefa wengi wa Tanzania waliwahi kutokota kabla yake na nitakumbushia baadhi ya mechi.
Machi 31, mwaka 2002 katika fainali ya Kombe la Tusker, Simba ikishinda 4-1, refa Abdulkadir Omar 'Msomali' aliivuruga mechi na kuvuruga amani uwanjani pia kwa madudu yake.
Kwa nini? Katika mechi hiyo ya fainali iliyohudhuriwa na rais mstaafu wa awamu ya pili ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ali Hassan Mwinyi, chupuchupu ivunjike dakika ya 32, baada ya Madaraka Suleiman kufunga bao ambalo kabla ya kufumua shuti lililomshinda kipa Manyika Peter, aliushika mpira kwa makusudi, ili kuuweka sawa.
Rais wa Yanga wakati huo, Tarimba Abbas aliinuka na kuwaonyesha ishara wachezaji wake watoke uwanjani na hapo ndipo meza kuu aliyokuwa ameketi mzee Mwinyi, ilipoanza kushambuliwa kwa chupa za maji na mashabiki wa Yanga. Abdulkadir Omar alisubiri hadi vurugu zilipotulizwa na FFU ndipo akaendeleza mchezo. Tarimba alitoka nje na hakutaka kuendelea kushuhudia mchezo huo. Baada ya hapo, alifungiwa na Chama cha Soka Tanzania, (FAT), sasa TFF kabla ya kujiuzulu uongozi wa klabu hiyo baadaye.
Agosti 18, mwaka 2002 Simba na Yanga zikitoka sare ya 1-1 katika mechi ya Ligi Kuu, refa Victor Mwandike aliwaacha mashabiki wa Simba midomo wazi kwa kuwapa Yanga penalti dakika ya 89 na ushehe, ambayo Sekilojo Chambua aliitumia vema kuisawazishia bao timu yake, baada ya Simba kutangulia kufunga kupitia kwa Madaraka Suleiman dakika ya 65.
Oktoba 24, mwaka 2007, refa Osman Kazi alikataa mabao matatu yaliyofungwa na Yanga, yote akidai kipa Juma Kaseja alisukumwa na wachezaji wa Yanga, lakini kwa yeyote atakayerudia kuangalia DVD ya mchezo ule, hawezi kuona ukweli wa madai ya Kazi.
Awali ya hapo, Kazi aliwahi kupuliza filimbi ya kumaliza dakika 45 za kipindi cha kwanza katika Nusu Fainali ya Kombe la Tusker mwaka 2005 mjini Mwanza, wakati mchezaji wa Yanga, Said Maulid 'SMG' amekwishawatoka mabeki wa Simba na anakwenda na mpira mbele yake amebaki Juma Kaseja tu.
Refa ni mwamuzi wa mwisho- lakini kwa wana Yanga walijutia mno tukio lile kwenye mchezo ambao mwishowe walifungwa 2-0, kwa mabao ya kipindi cha pili ya Emmanuel Gabriel na Mussa Mgosi.
Aprili 19, mwaka 2009, Jerry Tegete aliifungia Yanga bao la kusawazisha kwa mkono na kutengeneza sare ya 2-2, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Refa makini asingeweza kukubali bao lile, hivyo kwa haya yote lazima tukubali marefa wa Tanzania hawawezi tena kuchezesha mechi za watani wa jadi.
Sababu nyingine za marefa wetu kuzishindwa mechi hizo ni mapenzi yao kwa moja ya timu hizo, kitu ambacho Misri wamekiepuka na mechi ya Zamalek na Ahly inachezeshwa na marefa kutoka nje ya nchi yao.
Nakumbuka refa kutoka Uganda, Dennis Bate aliyechezesha Nusu Fainali ya Kombe la Tusker mwaka 2009 kati ya Simba na Yanga, aliiongoza vizuri mechi hiyo na akadhibiti ujanja wote wa wachezaji kutaka kumdanganya na hatimaye aboronge.
Kuna wachezaji wanaitwa wazoefu wa mechi za Simba na Yanga na hawa wamekuwa wakiwapoteza sana marefa kwa uzoefu wa kucheza mechi hizo, lakini kama marefa watatoka nje ya Tanzania, tena wa kiwango cha beji za FIFA, uhondo wa mechi za watani utaongezeka maradufu.
Zaidi ya mara mbili sasa naandika juu ya mechi za watani wa jadi kubadilishiwa marefa, lakini wakubwa wameendelea kukaa kimya- labda wanajua wanachokifanya, ila ukweli ulivyo kwa sasa, marefa wetu hawaziwezi tena mechi hizi.
Sioni kuna tabu gani TFF kualika marefa wa nchi jirani kuja kuchezesha mechi hii, ili kuondoa hofu kwa timu zote kabla ya kuingia uwanjani juu ya marefa. Wana hoja, kwa sababu uzoefu unawapa wazi kwa asilimia kubwa marefa wa hapa nyumbani huzishindwa mechi hizo, iwe kwa bahati mbaya, kurubuniwa au utashi.
Wadhamini wa Ligi Kuu, Vodacom wanataka ligi hii iwe bora na mfano wa kuigwa, sidhani kama hawatakuwa tayari kutenga bajeti ya marefa wa kigeni kwa ajili ya mechi mbili kila msimu.
Simba na Yanga, zote zinadhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager, ambao dhahiri wanataka nembo yao itangazwe na kitu chenye thamani na hadhi kubwa, sidhani kama hawatakuwa tayari kusaidia kuziwezesha mechi hizo za watani zichezeshwe na marefa wa nje. Kwa kifupi, sijui tatizo liko wapi.

Chanzo:http://bongostaz.blogspot.com
0 comments
 
Copyright © 2011. TANGA LEO - All Rights Reserved
Proudly powered by Blogger