Featured Post Today
print this page
Latest Post

PINDA, MAWAZIRI HATARINI KUNG'OLEWA

PINDA, MAWAZIRI HATARINI KUNG'OLEWA

Waziri Mkuu Mizengo Pinda pamoja na mawaziri wake wawili; Khamisi Kagasheki (Maliasili na Utalii) na Waziri wa Maendeleo ya Mifugo, Dk Mathayo David wameingia matatani kutokana na shinikizo linalowataka wang’oke katika nafasi zao.

Pinda pamoja na mawaziri hao wanatakiwa kuachia ngazi kama hatua ya kuwajibika kutokana na matukio ya vifo na baadhi ya watu kujeruhiwa, katika matukio ya migogoro ya wakulima na wafugaji kwa upande mmoja na utekelezaji wa Operesheni Tokomeza Majangili kwa upande mwingine.

Jana wabunge walicharuka na kuwataka mawaziri waliohusika katika Operesheni Tokomeza Ujangili wawajibishwe wakieleza kutoridhishwa na maelezo waliyoyatoa mapema jana, baada ya kipindi cha maswali na majibu.

Kelele za wabunge zilizuka baada ya wabunge kuanza kuchangia maelezo ya Serikali kuhusu migogoro ya wafugaji na wakulima, hifadhi za wawekezaji na maelezo ya Serikali kuhusu Operesheni Tokomeza Ujangili.

Aliyekuwa wa kwanza kuchangia mjadala huo ni Mbunge wa Kilolo, Profesa Peter Msola (CCM) ambaye katika hitimisho lake alitoa hoja ya kuundwa kwa Kamati Teule ya Bunge kuchunguza kile ambacho alikiita kuwa ni unyanyasaji wa wafugaji na uporaji wa mifugo yao.

Profesa Msola alielekeza shutuma zake kwa Serikali kuwa ilifanya operesheni zake kwa pupa bila kufanya maandalizi hivyo kuwaathiri wananchi wasiokuwa na hatia.

Spika wa Bunge, Anne Makinda kabla ya kuahirisha kikao cha Bunge jana mchana aliridhia kuundwa kwa Kamati Teule ya Bunge kwa ajili ya kuchunguza migogoro baina ya wakulima na wafugaji, wakati ‘madudu’ ya Operesheni Tokomeza Majangili yatachunguzwa kupitia Kamati ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira.

Chimbuko la hoja

Jana asubuhi kabla ya Bunge kuanza kikao chake, Spika Makinda alitoa taarifa kwamba Kikao cha Kamati ya Uongozi kingekutana wakati kipindi cha maswali na majibu kikiendelea, kwa lengo la kutoa mwelekeo wa mjadala wa hoja za dharura.

Hoja hizo ni zile zilizotolewa na wabunge wawili kwa nyakati tofauti; Alphaxard Kangi Lugora wa Mwibara (CCM) kuhusu Operesheni Tokomeza Majangili na Saidi Nkumba wa Sikonge (CCM), kuhusu vita baina ya wakulima na wafugaji.

Kamati hiyo ilikutana baada ya kipindi cha maswali na majibu na Spika Makinda alitoa taarifa za kusitisha shughuli nyingine, ili wabunge waweze kujadili masuala hayo ambako kabla ya kuanza mjadala aliwaita mawaziri kutoa taarifa zao.

Alianza Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Kagasheki ambaye katika maelezo yake alihitimisha kwa kutangaza kusitisha Operesheni Tokomeza ili kupitia mpango huo na kufanya maboresho ili kuondoa upungufu uliopo.


Licha ya kueleza sababu nyingi zilizofanya Serikali kuendesha operesheni hiyo, alisema ina manufaa makubwa katika kuokoa wanyama aina ya tembo, lakini waziri alihitimisha kwa kusema itakuwa ni busara kuifanyia tathmini wakati ikiendelea, hivyo kutangaza kuisitisha mara moja.

Kwa upande wake Dk Mathayo alitoa maneno ya kuomba radhi na kuwapa pole watu waliopatwa na usumbufu ikiwa ni pamoja na kupoteza mali zao na mifugo.

Mathayo aliwaeleza wabunge kuwa Serikali imepanga kujenga malambo katika maeneo mbalimbali kwa ajili ya kuwasaidia wafugaji kupata maji ili kupunguza safari za kuhamahama kutoka eneo moja kwenda jingine.

Shinikizo kwa Pinda

Baada ya kumaliza hotuba zao, wabunge kadhaa walipata nafasi ya kuchangia maelezo hayo huku wengi wakielekeza shutuma zao kwa mawaziri hao na wenzao wa Mambo ya Ndani ya Nchi na yule wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.

Wabunge wawili wa Chadema, Paulina Gekul (Viti Maalumu) na John Shibuda (Maswa Mashariki) walitaka Waziri Mkuu Pinda ajiuzulu kutokana kushindwa kwake kudhibiti mauaji na mateso kwa wananchi.

Gekul alisema kinachotokea sasa ni utekelezaji wa kauli ya Pinda aliyoitoa bungeni akisema wahalifu wapigwe tu pamoja na ile ya Kagasheki aliyoitoa mjini Arusha akisema majangili watakaokamatwa wamalizwe hukohuko kwenye hifadhi.

Mbunge huyo alieleza operesheni hiyo kwamba imesababisha mauaji ya watu wasio na hatia ikiwemo mama Emiliana ambaye alifuatwa akiuza nyanya, lakini akateswa hadi kufa na hadi sasa mwili wake bado uko katika Hospitali ya Babati baada ya wananchi kugoma kuuzika.

Shibuda kwa upande wake alisema Pinda anapaswa kufungua milango kwa mawaziri wanaotakiwa kujiuzulu haraka, kutokana na kulea uzembe ambao umesababisha madhara makubwa kwa wafugaji.

Shibuda alisema kuwa Wizara ya Mifugo imekuwa na mtazamo hasi lakini akasisitiza kuwa uzembe wa viongozi wa ngazi za mikoa, wilaya hadi vijiji unatokana na ukimya wa Pinda ambaye anashindwa kuchukua hatua yoyote dhidi yao.

Wabunge wengine

Kwa upande wake Nkumba aliunga mkono kuundwa kwa kamati teule, lakini akasisitiza kuwa mawaziri hao wanne wana hoja za kujibu ndani ya chama tawala CCM na kwa Rais, vinginevyo Serikali haipaswi kuendeshwa na viongozi wazembe wa aina hiyo.

-Mwananchi
0 comments

MARAIS MUSEVENI NA KENYATTA WAISHANGAA TANZANIA


MARAIS MUSEVENI NA KENYATTA WAISHANGAA TANZANIA

RAIS wa Uganda, Yoweri Museveni ametetea mazungumzo ya kile kinachoitwa ushirika wa hiari unaohusisha nchi tatu za Uganda, Rwanda na Kenya, huku akiishangaa Tanzania kuhusu madai yake ya kutengwa katika Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC). Museveni alidhihirisha mshangao wake huo jana mjini hapa, wakati akizungumza na waandishi wa habari baada ya kukamilika kwa mazungumzo yaliyowahusisha Rais wa Rwanda, Paul Kagame na Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta.

Katika kikao hicho, Museveni alidai majadiliano hayo ni sahihi kwa kuwa nchi hizo zinachojadili ni miradi ya miundombinu kwa ajili ya ukanda wa kaskazini.

Museveni alidai Tanzania itahusishwa wakati majadiliano yatakapohamia ukanda wa kusini, ambako ndiko lilipo taifa hilo lenye eneo kubwa zaidi miongoni mwa wanachama wa EAC.

Kauli kama ya Museveni pia ilitolewa na Rais Kenyatta wakati akizungumza na Wakenya waishio nchini Rwanda, akipuuza hofu iliyojengeka kuwa jumuiya hiyo inaelekea kuvunjika.

Rais Kenyatta alisema utekelezaji wa miundombinu ya kimaendeleo unaohusisha nchi hizo pamoja na Sudani Kusini, hauhujumu mtangamano wa jumuiya hiyo.

“Tumedhamiria katika malengo yetu ya mtangamano wa eneo hili na kulifanya listawi. Kwa sasa tunatarajia kaka na dada zetu wa Sudan Kusini kuungana nasi muda si mrefu na kuifanya EAC istawi na kuwa na nguvu zaidi,” alisema.

Aliendelea kueleza kwamba, tofauti na kinachoelezwa na ‘maadui’ wa mtangamano wa EAC, wanachama wote wa jumuiya hiyo bado wamedhamiria kuungana.

“Kutokana na wasiwasi wa majirani zetu, niliamua kuchukua hatua zilizofanikisha kupunguza siku za kusafirisha bidhaa kutoka Mombasa kwenda Kigali kutoka siku 22 hadi nane,” alisema.

Aidha alisema Serikali yake imeondoa vikwazo vyote vya usafirishaji mizigo na anatarajia mizigo itasafirishwa kwa kasi na urahisi zaidi katika nchi zote jirani.

Hata hivyo, viongozi hao walikwepa kuzungumzia suala nyeti zaidi ambalo nchi hizo katika mikutano miwili ya nyuma ziligawana majukumu ikiwamo kushughulikia suala la katiba ya shirikisho la kisiasa, viza moja, ushuru wa forodha na mengineyo ambayo yamo ndani ya mipango ya EAC.

Hivi karibuni, Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta alieleza msimamo wa Serikali ya Tanzania kutokana na kitendo cha nchi hizo kujiundia utatu wa hiari ndani ya EAC.

Akijibu moja ya maswali ya wabunge mjini Dodoma hivi karibuni kuhusu mwelekeo huo unaotishia mustakabali wa jumuiya hiyo, Sitta alisema Serikali imeamua kutohudhuria mikutano yenye ajenda ambazo nchi hizo tatu zimeshaweka msimamo wa peke yao. 

Sitta ambaye awali aliwahi kuonya kwamba kinachofanywa na nchi hizo ni kinyume na makubaliano na mkataba wa EAC, alienda mbali akisema Serikali imeshaanza mazungumzo na Burundi pamoja na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), ili kuanzisha ushirikiano wao.

Aidha alifafanua kauli ya hivi karibuni ya waziri mwenzake wa Mambo ya Nje, Bernard Membe, kwamba Tanzania inasubiri talaka, akisema yenyewe ndiyo yenye uwezo wa kutoa talaka kwa jumuiya hiyo kwa kuwa inamiliki asilimia 52 ya eneo lote, huku nchi zilizobakia zikigawana asilimia 48 iliyobakia.

“Hawa wenzetu wanafanya utoto wa kutuzunguka, sisi tunatumia hekima ya Mzee Mwinyi aliyesema ‘mwongo, mwongoze.’ Kama wao wana hila zozote juu yetu, siku si nyingi tutazibaini, kama ni ndoa ya kwenye jumuiya basi sisi ndiyo tutakuwa tumeoa. Hivyo tutatoa talaka sisi,” alisema.

Hata hivyo, Rais Museveni alipoulizwa na mmoja wa wanahabari wakati wa mkutano wake mjini Kigali, alidai kuwa hana taarifa ya malalamiko yanayotolewa na Tanzania kuhusu utatu wa nchi zao.

“Hadi nitakapopata barua rasmi kutoka Serikali ya Tanzania ndipo nitakapoamini, vinginevyo nahesabu kile ninachoshuhudia katika vyombo vya habari ni uongo,” alisema.

Hata hivyo, wanadiplomasia wa Tanzania wamekuwa wakieleza wasiwasi wao kuhusu kuachwa katika mipango ya jumuiya hiyo, wakisema haikualikwa kushiriki na wanatarajia kulifikisha suala hilo katika kikao cha wakuu wa EAC kitakachofanyika mjini Kampala, Uganda mwishoni mwa Novemba mwaka huu.
-Mtanzania
0 comments

Kamishna wa Magereza Tanzania, John Casmir Minja akabidhi vyeti vya udereva kwa mafunzo ya maaskari magereza

Kamishna wa Magereza Tanzania, John Casmir Minja akabidhi vyeti vya udereva kwa mafunzo ya maaskari magereza

Kamishna Jenerali wa Magereza Nchini, John Casmir Minja(mbele katika Jukwaa) akipokea Saalam ya heshima na Utii kutoka kwa Gadi Maalum ya Gwaride lililoandaliwa na Wahitimu 72 wa Mafunzo Maalum ya Udereva katika Chuo cha Magereza cha Ufundi na Udereva Kingolwira, kilichopo Mkoani Morogoro. Hafla fupi ya ufungaji Mafunzo hayo imefanyika leo Novemba 1, 2013 katika viwanja vya Kingolwira, Morogoro.

Kamishna Jenerali wa Magereza Nchini, John Casmir Minja  (kulia) akikagua Gadi Maalum ya Gwaride lililoandaliwa Maalum kwa ajili ya Ufungaji Mafunzo ya Udereva Kozi No. 19 ya Mwaka 2013 ambayo yamefanyika leo Novemba 1, 2013 katika Chuo cha Magereza cha Ufundi na Udereva Kingolwira, Mkoani Morogoro.


Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, John Casmir Minja akimkabidhi cheti mmoja wa Wahitimu wa Kozi ya Udereva, Cpl. Nuru kutoka Chuo cha Maafisa Magereza Ukonga, Dar es Salaam. Cpl. Nuru ni minongoni mwa askari 11 wa Kike ambao wamehitimu mafunzo Maalum ya Udereva leo Novemba 1, 2013  na Mafunzo hayo yamefanyika kwa muda wa Mwezi mmoja katika Chuo cha Ufundi na Udereva Kingolwira, Mkoani Morogoro ambapo jumla ya Askari 72 wamehitimu Mafunzo hao kwa ustadi mkubwa.
0 comments
 
Copyright © 2011. TANGA LEO - All Rights Reserved
Proudly powered by Blogger