Featured Post Today
print this page
Latest Post

MNEC AWATAKA VIJANA KUFANYA KAZI

                           

MNEC AWATAKA VIJANA KUFANYA KAZI



MJUMBE wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi Wilaya ya Tanga (MNEC), Kasimu Kisauji, amewataka walezi na wazazi wilayani humo kuwahimiza vijana kufanya kazi kwa bidii na kuacha kukaa vijiweni, hatua inayochangia kutumia muda mrefu kufikiria vitendo viovu.
Kisauji alitoa kauli hiyo hivi karibuni wakati akizungumza na vijana wa shina la Yebo Yebo, Kata ya Ngamiani Kusini jijini Tanga katika ziara ya Jumuiya ya Umoja wa Vijana Mkoa wa Tanga (UVCCM) iliyokuwa na lengo la kuupa uhai umoja huo.
Alisema iwapo vijana watakuwa mstari wa mbele kuwajibika kwa kufanya kazi itawasaidia kuwa na maisha bora ambayo yatawawezesha kuinua familia zao na jamii kwa ujumla, hali ambayo inachangia kuongezeka kwa pato lao.
Alisema vijana wamekuwa wakidanganyika kwa kuambiwa kuwa vijiweni ni sehemu ya kubadilishana mawazo, hatua inayowafanya waonekane kama ombaomba kila wakati.
“Maisha bora lazima yaendane na kufanya kazi na si kukaa vijiweni, vibarazani na kuanza kupiga soga zinazorudisha maendeleo nyuma,” alisema.
Akizungumzia suala la mikopo ya vijana na kina mama inayotolewa na halmashauri, Kisauji aliwataka vijana kuacha kulalamika badala yake wajiunge kwenye vikundi vitakavyowasaidia kuwezeshwa kupata mikopo hiyo.
Aliwataka  madiwani wa halmashauri ya jiji hilo kuhakikisha wanasaidia kina mama na vijana ili waweze kupata mikopo hiyo bila kuwepo usumbufu.
0 comments

MWANAMUZIKI FEROUZ AKAMATWA NA BANGI.

MWANAMUZIKI FEROUZ AKAMATWA NA BANGI.

Vijana ni nguvu kazi ya taifa, lakini vijana hao hao wanaweza kuwa chanzo cha taifa kutoendelea na
kubomoka. Ubomoaji wa taifa huwa kwa namna nyingi ikiwemo uvivu, ufisadi, na kadha wa kadha. Lakini hapa, tuangalie hili la madawa ya kulevya na bangi
Kila kukicha kuna wasanii wa maigizo na filamu ambao tunasikia
wamekamatwa na madawa ya kulevya, "unga" katika jitihada za 'kusaka maisha', wenyewe wanasema kuna ajali kazini. Wasanii hao ambao wengi ni vijana, na pale wanapoonekana kwenye runinga huwa hamasa kwa wadogo zao na jamii kwa ujumla, wakipenda kuwa kama wao.

Na mchana huu, maeneo ya Sinza, kuna taarifa ya mwanamuziki aliyetamba kwenye muziki wa bongo fleva, Ferouz, sanasana kwa wimbo wake wa Starehe, ambao ulikuwa ukionyesha madhara ya UKIMWI na virusi vya UKIMWI. Ferouz anadaiwa kukutwa na bangi, na picha ambazo Gospel Kitaa imezipata eneo la tukio, zinamuonyesha akisindikizwa na maafande kunako mbele ya vyombo husika.

Vijana wa Tanzania tuna shida gani? Kama ni ardhi tunayo, kama ni nguvu tunazo, sasa nini shida zaidi? Ipo haja ya Operesheni ambazo Askofu Sylvester Gamanywa ameitisha za Takasika iliyomalizika hivi karibuni, na kisha kupokelewa na Operesheni Milikisha, kuwahusisha pia wasanii wa aina zote, maana wanaonekana kukumbwa na janga hili kwa sana, vinginevyo, vijana ambao ndio nguvukazi ya taifa watakuwa wakijaa jela za ndani na nje, wakiacha wageni kuja kutawala.
0 comments

SHIRIKA LA UNDP LAMWAGA MAMILIONI KOROGWE VIJIJINI.

SHIRIKA LA UNDP LAMWAGA MAMILIONI KOROGWE VIJIJINI.

Korogwe SHIRIKA la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), limempatia Mbunge wa Jimbo la Korogwe Vijijini, Stephen Ngonyani 'Profesa Majimarefu' kiasi cha shilingi milioni 253 kwa ajili ya kukabili tatizo la maji katika jimbo lake fedha ambazo zimetokana na mfuko wa maendeleo vijijini.
Akikabidhi mkataba wa fedha hizo, Ofisa Miradi Shirikishi wa UNDP, Stela Zaarh amesema fedha hizo wamezitoa kwa wilaya hiyo kama jitihada za shirika hilo kusaidiana na Serikali kutatua kero zinazowakabili wananchi vijijini hasa suala la maji, afya na elimu.

Baada ya kupokea mkataba huo ambao fedha tayari zimeshaingizwa katika akaunti ya halmashauri ya wilaya kupitia mhandisi wa maji wa wilaya, mbunge huyo alisema kwamba fedha hizo zitachimba visima virefu katika vijiji vitano kata Majengo kilichopo kata ya Mswaha-Darajani, Makuyuni,  Kikwazu, Goha na Kwetonge.


Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri hiyo, Lucas Mweri aliyekuwepo kwenye makabidhiano hayo amesema mchakato wa kuwapata wakandarasi watakaochimba visima hivyo utaanza mara moja na kwamba sasa hivi hatua za awali za kuandaa mapendekezo ya mradi huo utaanza wiki ijayo.
Mkuu wa wilaya Korogwe, Mrisho Gambo aliyekuwepo pia kwenye hafla hiyo ya kukabidhi mkataba huo alimtaka mkurugenzi huyo kuhakikisha fedha hizo zinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa na kufika kwa walengwa ili kuondoa kero ya maji kwa wananchi na pia kuwashawishi waliotoa fedha hizo kutoa fedha nyingine.
0 comments

POLISI TANGA YAKUSANYA MILIONI 801.

POLISI TANGA YAKUSANYA MILIONI 801.

Na Oscar Assenga, Tanga
 
JESHI la Polisi Mkoa wa Tanga Kitengo cha Usalama barabarani, limeongeza makusanyo yanayotokana na makosa mbalimbali, kutoka Sh milioni 738.2 hadi kufikia Sh milioni 801.8. Ongezeko hilo ni la kuanzia mwaka 2012 na 2013, fedha ambazo zilitokana na makosa mbalimbali ya barabarani, baada ya uimarishwaji wa doria kwenye barabara kuu na za mijini.
Kamanda wa Kikosi cha Usalama barabarani Mkoa wa Tanga, Abdi Isango aliyasema hayo leo wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake, ambapo alisema fedha hizo zilikusanywa kutokana na makosa 26,178 yaliyopatikana mwaka jana na makosa 24,160 yaliyopatikana mwaka juzi.


Isango alisema makosa mengi yanatokana na ubovu wa matairi, kutokufunga mikanda na uendeshaji mwendo kasi ambao mara nyingi husababisha ajali na kupoteza maisha ya raia wasiokuwa na hatia kwa madereva wanaotumia barabara za Mkoa wa Tanga.

Aidha alisema takwimu za ajali za barabarani zimeonekana kupungua kwa kiasi kidogo, kutoka ajali 98 zilizojitokeza mwaka jana zilizosababisha majeruhi 219 ikiwemo watu 129 kufariki dunia kutokana na ajali hiyo, wakati mwaka juzi zilitokea ajali 98 zilizoua watu 104 ambapo ongezeko hilo ni sawa na vifo 25, ambayo ni sawa na asilimia 24 pamoja na majeruhi 153 ikiwa ni ongezeko la asilimia 66.

Akizungumzia ajali za pikipiki kati ya mwaka 2012-2013, Isango alisema ajali hizo zimepungua kutoka vifo 24 mpaka kufikia vifo 21, ambavyo ni sawa na ongezeko la asilimia 12.5 ambapo punguzo hilo limetokana na waendesha pikipiki wengi kupata elimu ya usalama barabarani na uimarishaji wa doria kwenye barabara kuu zote mkoani hapa.

Aliwataka wananchi kuacha kuendelea kutoa rushwa, kwa sababu kuendelea kufanya hivyo kunaweza kusababisha ongezeko la ajali za mara kwa mara barabarani, kwani wanapokuwa wakitoa rushwa askari wanashindwa kuwajibika ipasavyo na kuyaacha magari kuendelea na safari zake bila kujali madhara yatakayoweza kuwakuta.
0 comments
 
Copyright © 2011. TANGA LEO - All Rights Reserved
Proudly powered by Blogger