Featured Post Today
print this page
Latest Post

Wabunge 15 matatani

Wabunge 15 matatani

thomas1 e4385
Ofisi ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limewaanika wabunge 15, waliobainika kuchukua posho za safari bila kusafiri huku wengine wakikatisha safari zao.


Akizungumza katika mahojiano maalumu jana na mwandishi wa gazeti hili, Katibu wa Bunge Dk Thomas Kashililah, alisema tayari fedha hizo zimesharejeshwa kwa kukatwa kwenye mishahara yao.

Dk Kashililah alisema baadhi ya wabunge waliomba wasikatwe fedha hizo kwenye mishahara yao, badala yake wazirejeshe wao wenyewe.

Hata hivyo, Katibu huyo wa Bunge alisema wabunge hao walishindwa kusafiri kutokana na sababu mbalimbali, zikiwamo kuwa na ugeni wa viongozi wa chama na matatizo ya kifamilia.

"Kwa mfano Komba (Mbunge wa Mbinga Magharibi, John Komba) alishindwa kwenda kwa sababu ya kutembelewa na ziara ya Katibu wake wa Chama (Abdulrahman Kinana) muda wa safari ukamalizika hivyo akashindwa
kusafiri na taarifa zilikuwepo ofisini," alisema Dk Kashililah na kuongeza.


Akizungumzia safari ya Kiongozi wa Kambi rasmi ya upinzani, Freeman Mbowe nchini Uingereza, Dk Kashililah alisema Bunge halina uwezo wa kumzuia mbunge yeyote kufanya shughuli zake safarini baada ya kumaliza jukumu lililompeleka.

Dk Kashililah alisema Mbowe alikamilisha ziara yake ya Bunge na kwamba baada ya hapo aliendelea na shughuli za chama chake nchini humo.

"Suala hili lilikuwa limebeba hisia za kisiasa, baada ya kusikika tu bungeni basi vyombo vya habari vikaanza kuwahukumu wabunge ni mafisadi bila hata kutafuta ufafanuzi kutoka wetu. Sisi taarifa hizo tulikuwa nazo kabla ya hata ya kuibuka bungeni, lakini lilivyotafsiriwa sikupenda," alisema Dk Kashililah.

Dk Kashililahb alisema, "Bunge lilikuwa limeratibu jumla ya safari mbalimbali zilizokuwa zimependekezwa na Kamati 16, lakini hazikufanikiwa kwenda zote kwa pamoja.

Alisema ziara zote za kamati huandaliwa kwa mujibu wa kanuni ya 117 ambayo inazipatia mamlaka Kamati hizo kuandaa ziara inazooana zina manufaa kwa ajili ya kuboresha utendaji wake. Chanzo: mwananchi
0 comments

Dk Ngasongwa: CCM inababaika

Dk Ngasongwa: CCM inababaika


ngasongwa1 9cf74

Ni kutokana na viongozi wake kusema hadharani bila ya kutumia vikao vya chama

Dar es Salaam. Waziri wa zamani katika Serikali ya Awamu ya Tatu ya Rais Benjamin Mkapa na katika Awamu ya Nne ya Rais Jakaya Kikwete, Dk Juma Ngasongwa amesema kuwa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kinababaika katika kutekeleza majukumu yake.

Vilevile, chama hicho kimekumbwa mgawanyiko kati ya watendaji wake na Serikali na kwamba taifa lina ombwe la uongozi.

Kutokana na hali hiyo, Dk Ngasongwa ambaye pia ni kada wa CCM amemshauri Rais Kikwete kuwa mkali katika kusimamia watendaji wake anaowateua ndani ya chama na Serikali yake na kufuatilia na kupima utekelezaji wa yanayokubaliwa .

Alikuwa akizungumza katika mahojiano maalumu na gazeti hili nyumbani kwake mkoani Morogoro anakoendesha maisha yake kwa kilimo cha mpunga baada ya kustaafu.
Dk Ngasongwa alisema kuwa mgawanyiko huo kati ya watendaji wa Serikali na CCM, umeondoa umoja siyo tu katika vyombo hivyo, bali pia miongoni mwa wabunge wa chama hicho tawala.

Alisema kuwa hali hiyo inasababisha kutokea mambo mengi ikiwamo matukio ya mawaziri kushinikizwa kujiuzulu kama ilivyotokea hivi karibuni na kwamba kwa Serikali ya Awamu ya Nne hali hiyo imekuwa ikijirudia.
"Chama tawala kinababaika sana, tena hata watendaji wa CCM, wanawasema vibaya mawaziri hadharani, wakati wote ni wateuliwa wa Rais (Jakaya Kikwete) na ndiye mwenyekiti wetu wa CCM. Hii inakigawa chama. CCM ina utaratibu wake, kwa nini wasiitwe wakahojiwa ndani ya chama, badala ya kutajana hadharani:
"Sielewi kwa nini CCM inababaika. Inachotakiwa ni kuwa na mshikamano kwa wabunge wake kukutana mara kwa mara na kujenga msimamo. Hii ni kazi ya mawaziri na wabunge pia," alisema Dk Ngasongwa na kuongeza:
"...Tatizo uongozi haufanyi kazi vizuri, ndani ya chama chetu kuna mgawanyiko mkubwa hata katika Serikali, mfano Mwanasheria Mkuu (AG) anaposema baadhi ya mawaziri hawamsikilizi, hii 'No' (hapana), lazima kanuni za uendeshaji wa Serikali zifuatwe, hii ni muhimu."
Alisema hali hiyo inaonekana hata kwenye Baraza la Mawaziri na kwamba mgawanyiko pia upo ndani ya Bunge kwa wapinzani.

"Lakini kugawanyika kwa upinzani ni afadhali kuliko CCM, kwani matokeo yake ni kupunguza imani ya watu kwa Serikali yao na chama tawala," alisema.

Akinukuu maneno ya Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Dk Ngasongwa alisema: "Nyerere alisema, bila CCM madhubuti nchi itayumba na ndiyo yanayotokea sasa.

"Msingi wa yote yanayotokea ni ubinafsi, ubepari...; turudi kwenye Ilani ya chama, tuzungumze, tufikie mwafaka, siyo kutukanana hadharani. CCM itoe mwongozo siyo kugawa wananchi."
Ngasongwa aliyeshika nyadhifa mbalimbali za kisiasa katika CCM na Serikali ikiwamo ujumbe wa Kamati Kuu (CC), ubunge wa Ulanga Magharibi, Waziri wa Maliasili na Utalii na baadaye Waziri wa Mipango, Viwanda na Uwezeshaji, alifafanua kwamba kuna ombwe la uongozi katika chama tawala, upinzani, Serikali hata bungeni.

"Kuna ombwe la uongozi siyo tu kwa wapinzani, hata sisi chama tawala CCM, Serikali, hata bungeni pia kuna mchanganyiko na yanaonekana waziwazi. Tunaona Spika anavyodharauliwa na wabunge. Bunge linaonyesha picha ya hali halisi ya nchi yetu ilivyo,"alisema Dk Ngasongwa.
Alipotakiwa kuzungumzia zaidi
tukio la hivi karibuni la Rais Jakaya Kikwete kutengua uteuzi wa mawaziri wanne walioshinikizwa kujiuzulu kutokana na Ripoti ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Mazingira kuhusu Operesheni Tokomeza Ujangili, alieleza kuwa hajaisoma kwa undani ripoti hiyo, lakini inaonyesha kuwa utekelezaji wake ulikuwa mbaya.


Hata hivyo, alisema kuwa kamati hiyo ilitakiwa kuainisha makosa ya watendaji wa operesheni hiyo na kuwaacha mawaziri wajipime na kujiuzulu wenyewe.

Alisema kwamba hatua ya wabunge na kamati kushinikiza mawaziri hao wajiuzulu iliwachongea kwa Rais Kikwete aliyeamua kuwafukuza kazi kwa lugha ya kistaarabu, hali ambayo alielezea kuwa inaweza kujenga uhasama baina ya wabunge, kamati na mawaziri walioondolewa.

Hivi karibuni Rais Kikwete alitengua uteuzi wa Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Shamshi Vuai Nahodha, Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk Emmanuel Nchimbi pia Waziri wa Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi, Dk Mathayo David Mathayo baada ya wizara zao kutajwa kushindwa kusimamia Operesheni Tokomeza Ujangili, iliyopoteza maisha ya watu, mifugo na vitendo vya ukatili kwa binadamu.

Kuhusu kubadilika kwa mawaziri, Dk Ngasongwa alieleza kuwa jambo hilo siyo baya, lakini akasema kwamba likifanyika mara kwa mara linadumaza wizara kwa kukosekana mwendelezo wa utendaji.
 
"...Ikitokea mara kwa mara inadumaza utendaji, hupati 'continuity' (mwendelezo mzuri), kwani mawaziri huhitaji kujifunza na utekelezaji huhitaji muda. Continuity ni muhimu kwa mawaziri, hata watendaji wengine," alisema.

Hii ni mara ya tatu kufanyika kwa mabadiliko ya Baraza la Mawaziri tangu kuingia madarakani kwa Serikali ya Awamu ya Nne ya Rais Jakaya Kikwete, likiwamo lililotokea baada ya aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa kujiuzulu. Chanzo: Mwananchi
0 comments

JK kupokea Rasimu ya Katiba Mpya Jumatatu

JK kupokea Rasimu ya Katiba Mpya Jumatatu

 

Tume  ya Mabadiliko ya Katiba inatarajiwa kuwakabidhi Marais Jakaya Kikwete na Dk Mohamed Shein, rasimu ya katiba mpya.

Hafla ya makabidhiano hayo itafanyika Jumatatu, kwenye viwanja vya Karimjee, jijini Dar es Salaam.

Taarifa iliyotolewa jana jijini Dar es Salaam na Katibu wa Tume, Assaa Rashid, ilisema.

Akitoa ufafanuzi kuhusu kuendelea kuwepo kwa tume hiyo, Naibu Waziri wa Sheria na Katiba, Angela Kairuki, alisema tume itakabidhi nyaraka hizo na itaendelea na kazi.

Alisema itavunjwa kwa mujibu wa sheria baada ya rasimu hiyo kufikishwa na kusomwa kwenye Bunge Maalum la Katiba.

Taarifa ya Rashid ilieleza kuwa hafla hiyo pia inatarajiwa kuhudhuriwa na viongozi wa serikali, wa kisiasa, taasisi na asasi mbalimbali zikiwamo za kidini na kiraia pamoja na wananchi.

Taarifa hiyo ilisema Mwenyekiti wa Tume, Jaji Joseph Warioba, anatarajia kuwakabidhi Marais, ripoti ya mchakato pamoja na rasimu ya katiba mpya.

Rasimu hiyo imetokana na maoni ya wananchi, viongozi na makundi mbalimbali waliyoyawasilisha kwa tume kupitia njia mbalimbali zikiwamo mikutano ya hadhara, barua pepe, njia ya posta, tovuti (www.katiba.go.tz) na ukurasa wa facebook wa tume (Tume ya Mabadiliko ya Katiba Tanzania) na mabaraza ya katiba.

Mchakato wa kupata katiba mpya ulianza Julai, mwaka jana baada ya kuundwa kwa sheria ya kuanzisha tume ya mabadiliko ya katiba.

Kwa mujibu tangazo la Rais Kikwete kuhusu kuandikwa katiba mpya Tanzania inatarajia kuwa na katiba mpya ifikapo Aprili 2014, wakati wa maadhimisho ya miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

Baada ya kuundwa tume hiyo ilipewa miezi 18 ya kutekeleza jukumu la kukusanya maoni, kuyachambua na kutayarisha rasimu ya awali ili ijadiliwe na wananchi na kuandaa toleo hilo linalokabidhiwa kwa maraisi wiki ijayo.

Baada ya kuzunguka Bara na Visiwani Tume ilikusanya maoni kuyachambua na kutoa rasimu mpya iliyutoka  Juni mwaka huu na kujadiliwa kwenye mabaraza ya katiba ili kuiboreshwa zaidi.

Miongoni mwa mambo yaliyoibuliwa na rasimu ya awali ni kuwepo kwa serikali tatu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mapinduzi ya Zanzibar na Tanzania Bara.

Kadhalika ilizungumzia kuwepo kwa wagombea binafsi, kuondoa viti maalumu vya ubunge, kuweka ukomo wa ubunge na kuainisha mambo ya Muungano kuwa saba.

Bunge Maalumu
Kwa mujibu wa sheria ya mabadiliko ya katiba, baada ya kukabidhi rasimu hiyo ni kuitishwa Bunge Maalumu la Katiba.

Wajumbe wake wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, Wawakilishi kutoka Baraza la wawakilishi Zanzibar na wajumbe 166 watakaochaguliwa na kutoka asasi za kiraia, vyama vya siasa, taasisi za elimu ya juu, wafanyakazi, wakulima na makundi maalumu. 

Bunge hilo litaongozwa na Mwenyekiti ambaye ni kama Spika ambaye atakuwa na makamu na makatibu. Viongozi hao watachaguliwa kwa misingi ya Bara na Visiwani.
0 comments

Handeni wazitamani Simba na Yanga kukipiga kwenye Uwanja wa Azimio wilayani kwao

Handeni wazitamani Simba na Yanga kukipiga kwenye Uwanja wa Azimio wilayani kwao


Na Kambi Mbwana, Aliyekuwa Handeni

MKURUGENZI wa Halmashauri ya Mji wa Handeni, mkoani Tanga, Thomas Mzinga, amesema kwamba Uwanja wao wa Azimio unastahili kukutanisha vigogo vya Simba na Yanga, katika michuano yoyote nchini
 
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Handeni, Thomas Mzinga, pichani.
  Akizungumza na Handen Kwetu Blog mapema wiki hii wilayani Handeni, Mzinga alisema kuwa hiyo ni kutokana na maandalizi na mwonekano wa uwanja wao wa michezo.

Alisema kuwa Uwanja wao ni mkubwa na unastahili kukutanisha timu kubwa na vigogo wa Tanzania Bara, vikiwapo Simba na Yanga.

“Tunajivunia kuwa na uwanja mzuri na muwajulishe huko kuwa wanapaswa waje wacheze huku katika mashindano yao mbalimbali.

“Tunaamini Uwanja huu pia ukikamilika kwa baadhi ya ukarabati wake, basi utachangia kwa kiasi kikubwa kuleta watu mbalimbali, hasa timu kubwa zitakapokuja,” alisema Mzinga.

Hata hivyo, kiu ya Mzinga na viongozi wa serikali wilayani humo inaweza kutimia kama wataipigania au kuwashawishi viongozi wa Shirikisho la Soka nchini (TFF), kuhakikisha kuwa timu ya JKT Mgambo itaufanya Azimio kuwa uwanja wake wa nyumbani.
0 comments
 
Copyright © 2011. TANGA LEO - All Rights Reserved
Proudly powered by Blogger